YOUR MOST FAVORITE BLOG.

YOUR MOST FAVORITE  BLOG.
Calvin

Friday 19 June 2015

Mtoto ageuka bubu baada ya kung’atwa na mamba, Mbowe asema hajapoteza sifa na Utoro wakithiri bungeni…#MAGAZETINI JUNE19



headlineMWANANCHI
Hatua ya Jaji Mkuu wa zamani wa Tanzania, Augustino Ramadhani kujitosa kuchukua fomu za kuomba kuteuliwa na CCM kuwania urais imewavuruga wagombea wenzake wa urais na kuibua mjadala mzito katika maeneo mbalimbali nchini.
Mitandao ya kijamii ilijaa mijadala inayohusu kuingia kwake katika kinyang’anyiro hicho, huku baadhi ya wapambe wa wagombea wakieleza wazi kukatishwa tamaa na mgombea huyo ambaye wasifu wake unaonyesha ana sifa za ziada zaidi ya baadhi ya wagombea.
Miongoni mwa hoja zilizoibuliwa ni sifa ambazo CCM huzitumia bila kuzitaja, hasa kile kinachoitwa zamu kati ya Bara na Zanzibar na nyinginezo, ikielezwa kuwa akihitajika mgombea kutoka Zanzibar kumrithi Rais Jakaya Kikwete, Jaji Ramadhani anaonekana kufaa zaidi.
Katika mijadala hiyo, wapo waliohusisha hukumu alizowahi kuzitoa akiwa Jaji na baadaye Jaji Mkuu kwamba zililenga kukibeba chama hicho tawala kwa sababu anaonekana alikuwa na mapenzi nacho siku nyingi lakini wengine walieleza kuwa hawaoni tatizo kwa jaji huyo ambaye ni Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu.
Wakati maoni ya wananchi yakitofautiana juu ya hatua ya Brigedia Jenerali huyo mstaafu kuchukua fomu, mwenyewe aliliambia gazeti hili jana kwamba kwa sasa si jaji tena, hivyo ana haki ya kugombea urais na hakuna kanuni wala sheria inayomzuia.
Alitoa ufafanuzi huo baada ya kuulizwa swali kuhusu Ibara ya 113A ya Katiba ya Tanzania inayotajwa kumzuia, ikisema; “Itakuwa ni marufuku kwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu, Hakimu wa ngazi yoyote kujiunga na chama chochote cha siasa, isipokuwa tu kwamba atakuwa na haki ya kupiga kura iliyotajwa katika ibara ya 5 ya Katiba.”
“Ukisoma Ibara hiyo inasema kama mhusika ni jaji. Mimi huko nimeshaondoka sasa nitashindwa kugombea kwa lipi? Wacha watu waibue mambo tu, lakini hata ukisoma Katiba utaona mwenyewe wao wanazungumzia past tense (wakati uliopita), sasa tunazungumzia present tense (wakati uliopo),” .
Kuhusu mapenzi kwa CCM yanayoweza kuathiri utendaji, Jaji Ramadhani alihoji, “Hukumu gani niliipendelea? Hakuna kitu kama hicho.
Kuanzia 1961 tulivyopata uhuru, majaji hawakuwa kwenye chama? Sasa kuna ajabu gani mimi kuwa katika chama maana kipindi hicho kulikuwa na chama kimoja tu, watu wote walikuwa katika chama si majaji tu.
“Zamani (wakati wa chama kimoja), ulikuwa huwezi kupata kazi ya aina yoyote kama wewe si mwanachama. Leo ajabu ni mimi tu. Hata wanahabari ilikuwa lazima wawe wanachama.”
Jaji Ramadhani ambaye alikuwa Makamu Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, juzi mchana alichukua fomu kuwania nafasi hiyo ya kuongoza Serikali ya Awamu ya Tano huku akisema; chema chajiuza, kibaya chajitembeza.
Katika maelezo yake alisema alikuwa mwanachama wa Umoja wa Vijana wa Tanu tangu Agosti, 1969 wakati huo akiwa mwanafunzi wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
MWANANCHI
Siku moja baada ya kuhukumiwa kulipa faini Sh1 milioni au kwenda jela mwaka mmoja kwa kosa la shambulio la kawaida dhidi ya aliyekuwa mwangalizi wa ndani wa uchaguzi mkuu uliopita, Mbunge wa Hai na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe ametangaza kuwania tena ubunge katika jimbo hilo.
Mbowe aliyeepuka kwenda jela kwa kulipa faini hiyo juzi, alitangaza uamuzi huo jana alipokuwa akihutubia mkutano wa hadhara katika eneo la stendi ya zamani mji mdogo wa Bomang’ombe, Kilimanjaro.
Mwenyekiti huyo alifikia hatua hiyo baada ya wananchi waliojitokeza kwenye mkutano huo kumshinikiza agombee ubunge na kumchangia Sh800,000 za kuchukua fomu ambayo ndani ya Chadema hugharimu Sh250,000.
“Nashukuru kwa walioanzisha wazo hili lakini zaidi ninawashukuru waliojitolea kunichangia fedha. Nimekubali nitagombea ubunge katika uchaguzi ujao,” alitangaza Mbowe na kufanya uwanja kulipuka kwa shangwe.
Mbowe aliyeambata na wabunge kadhaa akiwamo Philemon Ndesamburo wa Moshi Mjini, alijinasibu kuibuka na ushindi wa kishindo yeye na chama chake katika uchaguzi ujao kuanzia jimbo la Hai na katika majimbo yote ya Mkoa wa Kilimanjaro.
“Kama sheria ingekuwa inaruhusu ningefurahi iwapo CCM ingesimamisha wagombea zaidi ya 10 katika Jimbo la Hai ili wapambane na mimi kwa sababu mgombea mmoja pekee siyo saizi yangu,” alijinasibu Mbowe.
Hukumu dhidi yake
Akizungumzia hukumu iliyomtia hatiani na kuhukumiwa faini au kifungo, Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Upinzani Bungeni alisema alikusudia kwenda jela kuwakilisha mamilioni ya Watanzania wanaosota huko “kwa kesi na hukumu za kipuuzi”.
“Kama kesi ya mtu mwenye dhamana ya uwakilishi wa wananchi kwa nafasi ya ubunge inaweza kuendeshwa kwa zaidi ya miaka minne na hukumu kutolewa katika mazingira tatanishi kama ilivyokuwa kwangu, Watanzania wa kawaida wanateseka kiasi gani?” alihoji Mbowe.
Alidai kuwa baada ya kumhukumu kifungo cha mwaka mmoja au faini ya Sh1,000,000, Hakimu Denis Mpelembwa amepandishwa cheo kuwa hakimu mkazi na kuhamishiwa mkoani Kagera, siku moja tu baada ya hukumu.
Kilichokuwa kinatafutwa ni namna ya kumzuia Mbowe asigombee ubunge Hai kwa sababu CCM wanajua nguvu yangu. Wamekosea sana kwa sababu hukumu ile hainizuii kugombea. Nitaombea na nitashinda kwa kishindo,” alisema.
HABARILEO
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe amesema hivi sasa nchi haihitaji Rais asiyetambulika nchi za nje kwani atapoteza muda mwingi kujitambulisha badala ya kushughulikia masuala mbalimbali ya wananchi wake.
Membe alitoa kauli hiyo mjni hapa jana wakati akizungumza na wanachama wa CCM waliomdhamini kwenye safari yake ya uhakika pamoja na wananchi waliokuja kumsikiliza.
“Tunataka Rais anayejulikana ndani na nje ya nchi si Rais ambaye atalazimika kupiga hodi kila nchi kujitambulisha kwani hatma ya Watanzania milioni 48 iko mikononi mwake,” alisema Waziri Membe na kuongeza;
“…Mtu kabla ya kuomba nafasi hiyo ya juu ya uongozi anahitaji kujiridhisha kwanza ndipo aweze kufanya uamuzi sahihi wa kuomba nafasi hiyo, mimi nimejipima nimejiona ninatosha kuwaongoza Watanzania katika masuala ya utawala bora.”
Alisema kuwa cheo cha urais hakijaribiwi kwani ni nafasi ya juu sana ambayo anayechaguliwa anapaswa kuangalia hatma ya nchi na watu wake.
Akiwa mkoani Singida, Waziri Membe alifanikiwa kupata wadhamini 1,905 idadi ambayo alisema si haba na kuwashukuru wananchi kwa moyo wa imani walioonesha kwake.
HABARILEO
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Anne Makinda amesikitishwa na wimbi la wabunge kutofika kwenye vikao vya mjadala wa bajeti ya serikali mwaka 2015/16.
Kwa kiasi kikubwa, hali hiyo inaelezwa inatokana na homa ya ubunge, wengi wakionekana kuelekeza akili zao katika majimbo yao ili kujiweka sawa na hatimaye warudi madarakani baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu.
Makinda ambaye aliongoza kikao cha juzi, ikiwa ni mwendelezo wa mjadala wa siku saba wa kuchangia mjadala wa bajeti, alijikuta akikosa maneno ya kuzungumza kutokana uchache wa wabunge wakati wa kuanza kikao cha jioni.
“Haya tuanze kuzungumza wenyewe sasa,” alisema Makinda kabla ya kumtaka Katibu wa kamati kusoma ratiba za shughuli za bunge kwa jioni hiyo ambapo wabunge waliokuwamo katika ukumbi wa bunge hawakuzidi 20.
Bunge lina zaidi ya wabunge 300. Alipokuwa akiahirisha bunge kwa siku ya juzi, Spika alisema: “Ninyi (wabunge) mnaobaki huko na kufuatilia majadala kwa kuangalia kwenye televisheni, sio vizuri.
Ni vyema kuwapo kwenye mjadala wa hii bajeti na kwa hili mtajifunza mambo mengi.” Wiki iliyopita alipokuwa akielezea mjadala wa bajeti kuwa utajadiliwa kwa siku saba, aliwaonya wabunge kutokuwa watoro katika vikao vya majadiano ya pamoja na kufahamu kuwa wabunge wengi wanajoto la uchaguzi.
Aidha, akichangia mjadala juzi jioni, Mbunge wa Viti Maalumu, Fakharia Shomar Khamis (CCM) aliitaka Serikali kuhakikisha inawachukulia hatua za kinidhamu ikiwa na kuwafukuza kazi watendaji ambao watakwamisha juhudi za kukusanya kodi.
“Hakuna haja ya kumhamisha mtendaji wa serikali ambaye atashindwa kukusanya kodi, maana kwenye utumishi kuna wafuasi wa CUF, CCM hata Chadema ambao wanaweza kuhujumu juhudi za serikali,” alisema.
Kuhusu tozo ya mafuta alitaka mafuta ya taa pia yapandishwe kwa Sh 50 kwa lita tofauti na mapendekezo ya serikali ya Sh 150 jambo ambalo litawaumiza wananchi wengi.
Mbunge wa Viti Maalumu, Maryam Msabaha (Chadema), aliitaka serikali kuhakikisha wanajizatiti katika kubana mianya ya biashara za magendo na bandari bubu, ili kuiwezesha TRA kukusanya mapato ya uhakika kwani kumekuwa na wimbi kubwa la watanzania kufanya biashara za magendo na kupitisha bidhaa kwenye bandari bubu linalokosesha serikali mapato.
JAMBOLEO
Penina Joseph mkazi wa kijiji cha Mrito Mkoani Mara amegeuka bubu baada ya kung’atwa na mamba.
Baba wa mtoto huyo Joseph Mngule alisema binti yake alishambuliwa na mamba Oktoba mwaka jana na hadi sasa hawezi kuzungumzo lolote.
Mungule alisema kabla binti yake hajashambuliwa alikua akizungumza kama kawaida huku akiendelea na masomo yake ya msingi lakini ba ada ya tukio aligeuka kuwa bubu na hivyo kushindwa kuendelea na masomo.
“Ukimwambia kitu anasikia na kutekeleza lakini hawezi kuzungumza, tuliambiwa na daktari huenda baadhi ya mishipa imekata mawasialino”Joseph.
Baba huyo alisema tangu kuugua kwa mtoto wake, tayari ametumia zaidi ya milioni 12 baada ya kuuza mali zake ili kuokoa maisha ya mtoto wake.
Pia alisema hilo sio tukio la kwanza kwa kijiji hicho kwani tayari watu sita wameuawa na mamba na wengine 30 kujeruhiwa huku ng’ombe, mbuzi na mbwa nao wakishambuliwa kwa wingi.
NIPASHE
Waziri mkuu wa zamani Edward Lowassa amezidi kupata ma elfu ya wadhamini huku akisema kutokana na wingi wa watu kujitokeza tayari ameshafunga magoli ya Urais.
Lowassa aliwasili jana katika Mkoa wa Kilimanjaro akitokea Tanga na kupata wadhamini 33,780 katika Mkoa huo.
Lowassa alisema anajivunia rekodi yake kwa Watanzania kutokana na kumjua na kujua nguvu yake katika utendaji kazi.
“Nadhani wale wenzangu 36 wakiona umati huu watajua na kujionea kuwa nimeshafunga magoli, tena magoli yenyewe ni sawa na yanayofungwa na kina Ronaldo na Messi hayana ubishi”Lowassa.
Alisema nia yake ya kugombea Urais ni kutokana na kujiamini, ana uwezo, anatosha na amegomea ili ateuliwe na chama hicho aweze kupambana na umaskini katika Taifa lenye rasilimali nyingi.
NIPASHE
Waandishi wa habari jana walizuiwa kuripoti kesi ya ugaidi inayowakabili viongozi 23 wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (JUMIKA), katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Washtakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo saa 3:15 asubuhi na kupelekwa kwenye chumba cha mahakama ya wazi namba moja wakiwa chini ya ulinzi mkali wa askari polisi na wale wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), waliokuwa wamebeba silaha na mabomu ya machozi.
Baada ya kuingia mahakamani hapo wakiwa wanamsubiri hakimu anayeisikiliza kesi yao, waandishi wa habari walijisogeza kutaka kuingia kwa lengo la kuripoti kesi.
Lakini cha ajabu, walipofika askari wa FFU waliokuwa wamebeba silaha na askari kanzu wa magereza waliokuwa wameuzingira ukumbi huo, waliwakataza waandishi kusogelea mlango wa kuingilia.
Hata hivyo, Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Inspekta Jackson Chidunda alidai kuwa upande wa mashtaka wameiomba mahakama na imeridhia kuwa kuanzia jana, waandishi wa habari hawapaswi kuripoti tena kesi hiyo kwa sababu za kiusalama na kiintelejensia.
Chidunda alidai kuwa ombi hilo lilitolewa mahakamani hapo na Wakili wa Serikali, Peter Njike mbele ya Hakimu Mkazi, Renatus Rutta kupitia kifungu cha 34 (4) cha Sheria ya Kuzuia Ugaidi ya mwaka 2002.
Kwa upande wa mawakili wanaowatetea washtakiwa hao, Ubaidu Hamidu na Abdulfattah Abdallah walidai kuwa upande wa mashtaka waliomba waandishi wa habari kuzuiwa kuripoti kesi hiyo kwa sababu inasadikiwa kuna watu wanarekodi na kwenda kurusha mwenendo wake katika mitandao ya kijamii, kitu ambacho ni kinyume na matakwa ya Mahakama.

No comments:

Post a Comment

gfjythfghgfhdfgergdfgbvdfgrfdgdfrgdrgdfrgrdegedrgdrfg