YOUR MOST FAVORITE BLOG.

YOUR MOST FAVORITE  BLOG.
Calvin

Tuesday 23 September 2014

ELEWA KUMUHUSU KAKOBE

TUNAENDELEA KUWALETEA MFULULIZO WA MAZUNGUMZO KATI YA ASKOFU KAKOBE NA MWANDISHI WETU kuhusu alipotokewa na yesu, mambo yalikuwaje?
Hii ndio nyumba ya Askofu Kakobe aliyoanzishia kanisa.
MJADALA NA MKEWE
Askofu Kakobe: Baada ya hapo nilijadiliana na mke wangu Hellen, nilimwambia nitashindwa kuhubiri au kuwa mchungaji. Sina maono kabisa ya kuanzisha shughuli ya kiroho, lengo langu ni kutumia fedha zangu kwa shughuli za kueneza wokovu wa Yesu Kristo. Nilimuambia mke wangu kwamba kama Yesu atanipa nafasi ya kuzungumza nitamuambia sitamani kuwa mchungaji au mhubiri, nitamuomba anipe uwezo wa kuwa tajiri ili niweze kuwasaidia wahubiri wa wokovu.
Mwandishi: Kwa nini uliamua hivyo?
Askofu Kakobe: Nilifanya uamuzi huo kujiunga na huduma kwa kutoa msaada katika Kanisa la Tanzania Assemblies of God. Nilimsaidia Askofu Moses Kulola kueneza mahubiri yake kwa kuyarekodi katika mitambo yangu ya kurekodia ya kieloktoniki na kusambaza kanda zake kwa watu kwa gharama zangu. Nikawa mmoja wa washirika wake. Kwa kweli sikupendelea kuwa mhubiri.
Mwandishi: Ukiwa unaabudu katika Kanisa la Assemblies of God, uliwahi kuhubiri angalau kwa siku moja kanisani?
Askofu Zakaria kakobe.
Askofu Kakobe: Hapana. Hata siku moja sikuwahi kuhubiri au hata kupewa jukumu la kufundisha dini, nilikuwa muumini wa kawaida tu.
Mwandishi: Ulipofanya uamuzi huo wa kutohubiri au kuwa mchungaji, Yesu hakukutokea tena?
Askofu Kakobe: Baada ya miaka michache alinitokea katika nyumba yangu (pichani juu) iliyopo Kijitonyama, Dar na alikuja kwa njia ileile kama alivyofanya mwanzo. Lakini safari hiyo hakuchukuwa muda mrefu. Alinieleza mipango ya Mungu kwangu na huduma nitakayotoa huku akitilia mkazo na akasema itachukuwa muda mrefu kunirudia tena na baada ya hapo, akatoweka.
Mwandishi: Ujio huo wa pili wa Yesu ulikubadili mawazo?
Askofu Kakobe: Hapana, niliendelea na mwenendo wangu uleule kwa miaka kadhaa. Lakini mwaka 1987 Novemba,  alikuja mhubiri maarufu wa kimataifa Reinhard Bonnke, alifanya mkutano mkubwa wa kiroho Dar es Salaam ambao uliwavutia watu wengi nami nilikuwa mmoja wapo, wengi wakajitoa kwa Yesu na miujiza mingi ilitokea pale (viwanja vya Jangwani).
Wakati mhubiri huyo anamalizia mahubiri yake, nilifikiria umati ule uliojitoa kwa Yesu ambao ulikuwa ni utukufu kwa Bwana katika jiji na kwa taifa kwa ujumla. Nikasikia sauti ikiniambia, ‘Mwanangu, mhubiri anaaga sasa, nani sasa atachukuwa nafasi yake? Nani atatangaza utukufu wangu baada ya huyu kuondoka?
Askofu kakobe akiwa na mkewe Hellen
ATETEMEKA MWILI MZIMA
Mwandishi: Sauti hiyo uliyoisikia bila shaka ni ya Yesu, je, ulifanya nini baadaye?
Askofu Kakobe: Sauti ile ilipasua moyo wangu na mifupa yangu ilianza kutetemeka, sikujiweza, wakati umati wa watu ukiimba nyimbo za kumalizia mkutano kwa furaha, mimi sikuweza kuimba nilikuwa nikilia sana kwa sauti ya juu. Nilijilaumu kwa kutotii agizo la bwana lakini nilimshukuru kwa kunivumilia, nikajitoa kwa Yesu na kumuambia Bwana kwamba nitumie mimi upendavyo.
Mwandishi: Ikawaje baada ya kujitoa rasmi kwa Yesu?
Askofu Kakobe: Moyo wangu ghafla ukajazwa Roho Mtakatifu, nikavutiwa katika kupenda kuhubiri Neno la Mungu na kuombea wagonjwa na wenye mahitaji. Sikungoja tena hata siku moja kuingia katika kazi ya bwana, yaani kuhubiri na kuingia katika miujiza ya uponyaji.
KUANZA KUHUBIRI RASMI
Mwandishi:  Kwa hiyo baada ya hapo ukawa mhubiri wa Neno la Mungu?
Askofu Kakobe: Ni baada ya maandalizi ya kiroho, siku ikafika Agosti 3, mwaka 1988, nikaanza rasmi safari yangu ya kuhubiri utukufu wa Mungu na timu iliyokuwa ikiitwa The Gospel Evangelistic Team (GET). Nilienda na timu hiyo mikoani na kuanza mikutano ya uponyaji baada ya kualikwa na makanisa ya Kipentekoste.
Nilifanya mikutano kumi sehemu za wazi katika Miji ya Tanga, Kilimanjaro, Tabora, Mbeya, Pwani na Dar es Salaam.
Mwandishi: Nini maoni yako kuhusu mikutano hiyo kumi ya mwanzo?
Askofu Kakobe: Baada ya mikutano hiyo nakumbuka mchungaji mmoja mwandamizi alisema, mikutano hii imethibitisha wito niliopewa na Mungu. Katika mikutano hiyo watu waliohudhuria walikuwa wengi kuliko matazamio yetu. Watu wengi wakaamua kumfuata Yesu na katika mikutano yote miujiza ya uponyaji ilitokea.

No comments:

Post a Comment

gfjythfghgfhdfgergdfgbvdfgrfdgdfrgdrgdfrgrdegedrgdrfg